Uteuzi wa Wagombea
Siku ya Uteuzi
Siku ya Uteuzi wa Wagombea Urais, Ubunge na Udiwani hupangwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi. Wagombea uchaguzi katika
ngazi zote sharti wawe ni wanachama wa Chama cha Siasa na wawe wamependekezwa na Vyama vya Siasa kwa maandishi. Kwa
uchaguzi wa mwaka 2005 uteuzi wa wagombea utafanyika tarehe 20 Agosti 2005.
Mamlaka zitakazoshughulikia uteuzi wa wagombea ni kama ifuatavyo:
- Mgombea Urais na Umakamu wa Rais - Tume ya Taifa ya Uchaguzi
- Mgombea Ubunge - Msimamizi wa Uchaguzi
- Mgombea Udiwani - Msimamizi wa Uchaguzi au Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi
Wajibu wa Vyama vya Siasa, Wagombea na Mawakala
Wajibu wa Vyama vya Siasa
- Wajibu wa Vyama vya Siasa ni kupendekeza wagombea wa Vyama vyao. Ni vizuri Vyama navyo vijiridhishe kwamba wagombea
wanaowapendekeza wanazo sifa zote zinazotakiwa kwa mujibu wa Sheria. Chama kikishampendekeza mgombea kimpatie mgombea
huyo barua ya kumtambulisha rasmi kwa Msimamizi wa Uchaguzi. Vyama ambavyo vina mgawanyiko wa uongozi, vihakikishe kwamba
fomu za mgombea wao zinatiwa saini na viongozi wa kitaifa kwa wanaogombea nafasi ya Ubunge na Uongozi wa Mkoa kwa upande
wa Wagombea Udiwani ngazi ya Kata. Uongozi wa kitaifa ni ule unaotambuliwa na Msajili wa Vyama vya Siasa.
Wajibu wa Wagombea
- Kuhakikisha na kujiridhisha kwamba wanazo sifa zote zinazotakiwa kwa mujibu wa Katiba na Sheria za Uchaguzi, na
kwamba hawajaondokewa na sifa yoyote.
- Kuelewa barabara aina za fomu zote zinazohitajika kwa uteuzi rasmi; zinapatikana wapi na kwa masharti gani;
zinatakiwa kurudishwa lini, wapi na kwa masharti gani. Fomu zinapatikana kwa Msimamizi wa Uchaguzi na zinarudishwa kwa
Msimamizi wa Uchaguzi au Tume ya Taifa ya Uchaguzi. Zile zinazohusu uchaguzi wa Wabunge na Madiwani zinarudishwa kwa
Msimamizi wa Uchaguzi na zile zinazohusu uchaguzi wa Rais zinarushwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi.
- Kuzielewa haki zao, pamoja na masharti na utaratibu wa uteuzi. Haki hizo ni pamoja na kutoa pingamizi kwa Msimamizi
wa Uchaguzi dhidi ya uteuzi wa mgombea yeyote, na kukata rufaa kwa Tume dhidi ya uamuzi wa Msimamizi wa Uchaguzi
kuhusu pingamizi.
Utaratibu wa kushughulikia wapigia kura wanaodhamini mgombea zaidi
ya mmoja
Mpiga kura aliyeandikishwa, ataruhusiwa kumdhamini mgombea mmoja kwa kila uchaguzi. Kwa uchaguzi wa Rais, Wabunge na
Madiwani mpiga kura mmoja anapodhamini zaidi ya mgombea mmoja kwa kila uchaguzi na wagombea hao wakateuliwa na Msimamizi
wa Uchaguzi, udhamini huo hautabatilisha uteuzi wa wagombea waliodhamini isipokukwa itakuwa ni kosa la jinai kwa mpiga
kura aliyedhamini wagombea hao.
Mpiga kura aliyedhamini mgombea zaidi ya mmoja akikubali kosa kwa maandishi, Msimamizi wa Uchaguzi anawaweza kutoa
adhabu ya kumtoza faini isiyozidi Shs 200,000/=. Mpiga kura akikataa shauri hilo litapelekekwa Mahakamani na
Msimamizi wa Uchaguzi.