Pingamizi dhidi ya Uteuzi wa Mgombea Udiwani
Wanaoruhusiwa kutoa pingamizi
- Mgombea yeyote wa Kata ya mgombea anayepingwa
- Msimamizi wa Uchaguzi/Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi
Mtu mwingine yeyote haruhusiwi kutoa pingamizi.
Muda wa kutoa pingamizi ni baada ya saa kumi (10.00) jioni ya siku ya Uteuzi mpaka saa kumi (10.00) jioni ya
siku inayofuata.
Sababu za Pingamizi
Sababu ya pingamizi inaweza kuwa yoyote kati ya zifuatazo, kwamba:
- Maelezo yaliyopo katika fomu ya uteuzi hayatoshi kumtambulisha mgombea;
- Fomu ya Uteuzi haitimizi au haikuwasilishwa kwa mujibu wa masharti yaliyowekwa na Sheria;
- Kutokana na maelezo yaliyoandikwa katika fomu ya uteuzi ni dhahiri kwamba mgombea uchaguzi hana sifa
zinazotakiwa;
- Uthibitisho wa Msimamizi wa Uchaguzi unaopaswa kutolewa haukutolewa;
- Hakuna picha ya mgombea;
- Hakuna uthibitisho kuwa mgombea amelipa dhamana shilingi Elfu tano (5,000/=).
Uamuzi wa Msimamizi wa Uchaguzi
Msimamizi wa Uchaguzi au Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi mara baada ya kupokea pingamizi anatakiwa amuarifu kwa
maandishi mgombea anayepingwa juu ya pingamizi hiyo na kumtaka atoe maelezo yake juu ya hiyo pingamizi.
Mgombea anayepingwa atoe maelezo ya kujibu pingamizi hiyo akipenda kwa Msimamizi wa Uchaguzi mapema
iwezekanavyo.
Baada ya kupata taarifa za pande zote Msimammizi wa Uchaguzi au Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi anaweza kuendelea
kutoa uamuzi wake. Hata kama anayepingwa hatatoa majibu, Msimamizi wa Uchaguzi anaweza kutoa uamuzi wake.
Rufani Dhidi ya Pingamizi
Msimamizi wa Uchaguzi au Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi amwelekeza aliyetoa pingamizi, kukata rufaa kwa Tume ya Taifa
ya Uchaguzi endapo hakuridhika na uamuzi wa Msimamizi wa Uchaguzi au Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi katika muda wa saa
48 tangu kutolewa kwa uamuzi wa Msimamizi wa Uchaguzi au Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi. Rufaa itawasilishwa kwa
kutumia Fomu namba 12.
Uamuzi wa Tume
Uamuzi wa Tume kuhusu rufani utakuwa ni wa mwisho na ambaye hataridhika nao, anaweza baada ya uchaguzi,
kufungua malalamiko ya uchaguzi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi.