JIANDAE KUSHIRIKI UCHAGUZI MKUU 2010
Mwaka 2010 ni mwaka wa uchaguzi. Ni mwaka ambao wananchi watafanya maamuzi baada ya kufanya tathmini juu ya ni kwa kiasi gani malengo na matarajio ya Watanzania yamefikiwa. Ni muda ambao Watanzania wataamua ni kwa kiwango gani wamefikia maisha bora kwa kila Mtanzania kama walivyoahidiwa na Chama tawala, Chama cha Mapinduzi, CCM.
CHADEMA tunawaomba Watanzania wajiweke tayari kufanya mabadaliko kwani tunaamini kuwa ahadi zilizotolewa ilikuwa dhana tu na kwamba mabadiliko ya kweli hayawezi kufanywa na viongozi walewale, wa chama kilekile, chenye uoza uleule, wakiendeleza yale yale, eti kwa Ari , Nguvu na Kasi mpya. Tanzania inahitaji mabadiliko ya mfumo yatakayozaa ukombozi wa fikra.
CHADEMA tunaamini katika Nguvu na Mamlaka ya Umma. Tunaamini kuwa mabadiliko ya kweli na Uhuru wa kweli haviwezi kufikiwa isipokuwa kwa kufanya mabadiliko ya mfumo na kuwa na uongozi thabiti , uongozi wenye maadili, kuwa na viongozi wanajali na kuheshimu matakwa ya binadamu wenzao. Viongozi wanaomuogopa Mungu ili kupambana na ufisadi na uoza unakaribia kuliangamiza taifa hili.
Matatizo ya taifa hili yanamgusa kila mzalendo mwenye uchungu na unyonge wake na unyonge wa jirani yake. Hivyo ni jukumu lako ewe mzalendo wa nchi hii kuanza kujiandaa kwa tukio adhimu kabisa, tukio la uchaguzi, tukio la kubadilisha uongozi na hatimaye mfumo wa nchi hii.
Ni wajibu wako ewe mzalendo mwenye wito wa uongozi kushiriki kwa kugombea. Ni wajibu wako ewe mzalendo mwenye kiu ya uongozi bora kuwashawishi wenye wito wa kuongoza wagombee. Ni wajibu wa kila mzalendo wa nchi hii kuanza maandalizi ya kufanya mabadiliko ya nchi hii kwa kuchangia kwa hali na mali.
Hakuna ufalme uliodumu milele isipokuwa wa Mungu pekee. CCM imepoteza uongozi imebaki na utawala. Ni wajibu wetu sasa kuipumzisha kwani uchovu wa chama tawala ni angamizo kwa watawaliwa.
Chukua hatua sasa, anza kujiandaa leo! Mabadiliko ni mchakato. Ni vema kama mzalendo uanze kujiandaa ili kwa pamoja tujenge taifa lenye matumaini. Taifa lenye TUMAINI JIPYA.