lf.bevel
MWANZO CHAMA SERA KATIBA TUUNGE MKONO UCHAGUZI TUWASILIANE
banner
Mengineyo
»Matamko mengine
»Habari Mpya
»Makala mbalimbali
»Midahalo
»Blogu za wanachama
»Picha za matukio
»Maoni Yenu
b.part
Barua Pepe
jina la mtumiaji:
neno-siri
rt.bt.spc
bt.part2


Tamko la Mkurugenzi wa Vijana wa Taifa wa CHADEMA kuhusu kauli ya Serikali ya Kuwakana Vijana wa Kitanzania waliotelekezwa Ukraine

"Nimesikitishwa na kauli ya serikali ya kutangaza kutowatambua vijana hawa wa kitanzania wakati ambapo vielelezo mbalimbali vilivyotolewa na wazazi wa watoto hao vinaonyesha kuwa walikuwa na baraka za serikali wakati wa kuondoka kwao. Aidha inashangaza kwamba pamoja na suala hili kufikia hatua ya juu kwa maana ya kufahamika na Rais Kikwete, Waziri Mkuu Lowasa na hata balozi mbalimbali, kauli ya kutowatambua imetolewa na mtendaji wa serikali. Tulitegemea Waziri mwenye dhamana ya wizara hii angejitokeza sasa kutoa ufafanuzi kuhusu suala zima. Hii ni ishara ya kukosa uwajibikaji. Sijui Waziri Msolla anafanya kazi ya kuwatumikia walipa kodi wa nchi gani kama masuala yanayowahusu watanzania yanayoigusa wizara yake anakwepa kutolea ufafanuzi. Alikuwa kimya katika kipindi cha mgomo wa vyuo vikuu vya SUA na UDSM. Sasa yuko kimya tena katika suala la wanafunzi wa kitanzania waliotelekezwa Ukraine. Na uko ushahidi kwamba amekuwa akikata simu akipigiwa kuulizwa kuhusu suala hili. Vijana wa CHADEMA tunaunga mkono kauli iliyotolewa na viongozi wakuu wa upinzani ya kumtaka Profesa Msolla ajiuzulu mara moja. Mfumo mzima wa uchangiaji wa elimu ya juu na utendaji wa bodi ya mikopo unaliingiza taifa kwenye malumbano yenye hasara kwa wanafunzi na nchi kwa ujumla; hivyo yeye kama waziri wa wizara inayohusika na suala hili anapaswa kuwajibika. Hivi kwani hakuna watanzania wengine wenye kuweza kuendesha wizara ya elimu ya juu zaidi yake?

Rais Jakaya Kikwete aunde tume huru ambayo itapewa mamlaka ya kuchunguza ukweli wa madai ya vijana hawa na kuchukua hatua mara moja ya kutatua suala hili. Pendekezo linalotolewa ni kuwa, kabla ya lolote kufanyika serikali ikubali kuwadhamini vijana hawa kwa mwaka ujao wa masomo (kwani tayari wameshaanza masomo miezi hii yote) na iachane kabisa na wazo la kuwanunulia tiketi warudi nyumbani. Wazo la kuwarudisha nyumbani ni wazo la watu walioshindwa! Endapo vijana hawa watarudi nyumbani itakuwa ni ishara ya viongozi wetu kushindwa kabisa kutatua matatizo na badala yake kung'ang'ania visivyong'ang'anika. Kama tumeweza kuvumilia na kuwapa muda watendaji wengi wabovu wajirekebishe, nina uhakika serikali inaweza kabisa kuwavumilia na kuwadhamini vijana hawa kwa mwaka huu wakati tume inachunguza ukweli. Tume iwe na uhuru na uwezo wa kumuita na kumhoji kiongozi yeyote na ifanye kazi zake mbele ya vyombo vya habari. Endapo baada ya uchunguzi kufanyika itagundulika kuwa kuna makosa yalifanyika basi serikali inaweza aidha kuwaambia vijana hivyo lakini kuendelea kuwasomesha hadi wahitimu kwa makubaliano mapya au kuwarudisha nyumbani kwa mpango wa kuwapa nafasi ya kuendelea na masomo yao nyumbani. Kwa kufanya hivyo wanafunzi hawapotezi, na serikali haishindwi.

Na endapo itaonekana kuwa viongozi kule bodi ya mikopo na wizarani waliboronga basi hatua za kinidhamu zichuliwe dhidi yao. Jambo la maana ni kuunda tume huru ambayo itakuwa na uwezo wa kumhoji kiongozi yeyote hadharani na kuita vielelezo vyovyote. Kwa kufanya hivyo, serikali itaonesha kulipa uzito unaostahili suala hili badala ya kutulazimisha tukubali matamshi yake tu hata kama matamshi hayo yanazua maswali zaidi kuliko majibu.

Ni matumaini yangu kuwa serikali itaonesha busara na si papara na itatumia hekima ya hali ya juu ili kuhakikisha kuwa vijana wetu wanaendelea na masomo, taratibu zinafuatwa na Taifa letu linaendelea kuheshimu elimu ya juu bila ya kujali hadhi au hali ya mtu.

Hili tatizo linafanana sana na tatizo lililo wakumba wanafunzi wa Tanzania nchini Poland mwaka 1996/97. Mtu aliyekuwa anawakwamisha ni Prof. Mahalu,Wakati hupo akiwa mkurugenzi wa elimu ya juu. Na wenyewe waliambiwa hivyo hivyo hawatambuliwi na warudi nyumbani. Waliorudi ndio hawakusoma tena labda baadaye sana. Kuna vijana wengine wakazamia Magharibi. Bahati nzuri baada ya kama mwaka tatizo lao likatatuliwa na wote waliokuwa bado wako Poland, wakasoma na sasa wamemaliza masomo na wanaitumikia serikali yao.

Jitihada zifanywe ili hawa wanafunzi wamalizie masomo yao huko huko waliko maana wakirudi Tanzania kwanza kwa mwaka 2007/8 hawawezi kwenda vyuoni maana muda umepita. Hata huko mbele itakuwa ngumu na itabidi wagombanie hizo nafasi na wanafunzi wengine wa miaka ijayo.

Hata kama kuna kosa limefanyika, suluhisho rahisi ni kuwasaidia hao vijana wamalizie masomo yao huko huko Ukraine.

Kwa kuwa hali ya wanafunzi kule Ukraine ni mbaya, natoa rai kwa watanzania wenye mapenzi mema walione jambo hili kuwa ni janga linalohitaji misaada ya kibinadamu. Wakati jambo hili linatafutiwa ufumbuzi lazima tuchukue hatua za kuokoa maisha ya watanzania wenzetu. Hapa natarajia mashirika yanayohusika na haki za binadamu yataangalia swala hili kwani vijana wale wanaishi kwenye mazingira magumu sana na hili linahatarisha hata mustakabali wa maisha yao kwani huenda wengine wakapatwa na matatizo ya kiakili na kuamua kufanya jambo lolote ambalo nlitayahatarisha maisha yao. Natoa mwito kwa watanzania kuchangia harambee ambayo viongozi wa vyama vya upinzani wameomba shirika lisilo la kiserikali la TANLET liratibu kwa ajili ya kuwaokoa vijana hawa wa kitanzania wasikose elimu.

Mwisho narudia tena rai ya kuitaka Wizara inayohusika kuendesha mjadala kuhusu Uchagiaji wa Elimu ya Juu nchini kabla ya Bunge kujadili bajeti ya Mwaka wa Fedha 2007/2008 ili kuepusha migogoro katika vyuo vya elimu ya juu nchini ambayo kwa kiasi kikubwa inasababishwa na suala hili. (Rejea taarifa ya Tume iliyoundwa na serikali miaka ya hivi karibuni kuchunguza vyanzo vya migomo na migogoro katika elimu ya juu). Baadhi ya mambo muhususi yanayopaswa kushughuliwa ni: Mifumo ya Uchangiaji wa gharama za elimu ya juu; Kusitisha mapendekezo ya mabadiliko ya Sheria na. 9 ya mwaka 2004 yenye kulenga kuimarisha uwekaji wa madaraja na viwango vya asilimia katika uchangiaji wa elimu juu; Haja ya kupandisha madaraja ya utoaji mikopo na kuweka stahili ya mikopo kwa wote wenye kupata udahili (admission); mifumo ya kutambua uwezo wa wanafunzi (means testing); Kiwango cha ruzuku na menejimenti/uendeshaji wa bodi ya mikopo na mifumo ya urejeshaji wa fedha za mikopo kwa wanafunzi. Tuko tayari kutoa maoni yetu ya ziada pindi utaratibu utakapotangazwa. Mabadiliko yaliyotangazwa na bodi ya mikopo hivi karibuni ya kuweka viwango vipya vya mikopo bado hayajajibu hoja za wanafunzi, wazazi na wadau wa elimu nchini. Bado serikali imeendeleza utaratibu wenye kuchochea madaraja na matabaka katika elimu ya juu nchini hivyo mjadala kuhusu suala hili ni jambo linalohitaji kufanyika mapema iwezekanavyo. Tunaweza kuona suala la watanzania 29 waliotelekezwa Ukraine ni jambo dogo; lakini linabeba ujumbe mzito kuhusu mapungufu yaliyomo katika mfumo wetu wa elimu ambayo yapaswa kushughulikiwa kwa hatma ya Taifa letu"

Tamko hili limetolewa tarehe 29 Mei 2007:

John Mnyika
Mkurugenzi wa Vijana

lf.curl lf.curl2 rt.curl2 rt.curl