lf.bevel
MWANZO CHAMA SERA KATIBA TUUNGE MKONO UCHAGUZI TUWASILIANE

Kufukuzwa kwa Wakulima Mbarali

na
Edwin I.M. Mtei

Nimeona majibu ya Mhe. Mungai, Waziri wa Kilimo kuhusu hoja yangu juu ya suala la Wakulima wa Mbarali. Ameyachapisha kama matangazo ya kulipia katika magazeti mengi ya tarehe 4 Agosti, 2006, nahisi ili kuweka bayana yote yahusuyo suala hili. Kwa vile mimi sina uwezo kifedha kuchapisha ufafanuzi wangu kama tangazo, naomba wahariri wanaotaka haki itendeke, wachapishe jibu langu hili kama taarifa ya habari ya kawaida.

Kwa kifupi, katika makala yangu iliyotangazwa na gazeti la ThisDay, nilishauri kuwa badala ya kuwafukuza maelfu ya wakulima walioharibu mazingira Mbarali, Serikali ingepeleka huko wahandisi wa maji na wataalamu wa kilimo kufundisha na kusimamia hawa kulima juu ya matumizi bora na endelevu ya maji na ardhi. Nilisisitiza kuwa jukumu na wajibu wa Serikali ni kuhakikisha kwamba wananchi wengi iwezekanavyo wanatumia mazingira yao kwa njia endelevu badala ya kuwaondoa na kuwapa wachache na wageni, ardhi ambayo Mwenyezi Mungu amewapa. Nataka kurudia kwamba Serikali itakuwa inakiuka wajibu wake ikifanya hivyo; na itakuwa imepoteza huruma na uzalendo wake, na kwa hiyo kustahili kuondolewa madarakani kidemokrasia. Nasisitiza pia kwamba sio wakulima wa Mbarali pekee yao wameharibu mazingira na jawabu ni kuwasaidia waendeleze mashamba yao kisayansi badala ya kuwaondoa.

Nilimalizia hoja yangu kwa kushauri wapinzani waungane na wakulima wa Mbarali katika maandamano ya amani kwenda kumsihi Rais wetu, Mhe Jakaya Kikwete asitishe mpango huu wa kuwafukuza kutoka katika ardhi waliolima kwa muda mrefu katika nchi waliopewa na Mwenyezi Mungu. Siyo kweli kwamba mimi ninawashawishi wakulima hawa waandamane. Wao wenyewe, walitangaza nia yao ya kuandamana kwenda Ikulu, kumwomba Rais wao aingilie, baada ya kutoridhika na majibu ya Serikali walipokwenda Dodoma. Na mimi nasema ingefaa wapinzani wawaunge mkono. Mhe. Mungai anaona kwa hilo mimi ni mchochezi! Kwa mtindo huu, Watanzania wengi watakuwa ni wachochezi kwa vile hawakubaliani na hatua za Mhe. Mungai.

Nimeona na kusoma maelezo ya Mhe. Mungai. Ni kweli kuwa mashamba haya yalikuwa yanalimwa na shirika la umma (NAFCO) wakati nikiwa Gavana wa Benki Kuu na hata nilipokuwa Waziri wa Fedha. Kutokana na kushindwa kwa NAFCO, wananchi binafsi walirudia kulima sehemu walizokuwa wanalima hapo awali na Mhe. Mungai anasisitiza kuwa “walikodishiwa”. Ninavyoelewa ni kuwa wale wanaolalamika kwamba waendelee kuyalima, wameyalima kwa takriban miaka kumi. Na nasema kwamba kama Serikali ingewapa msaada wa ugani wa maofisa wa Kilimo na wahandisi wa maji, wangeendelea kulima mpunga kwa kutumia miundombinu kama mifereji ya umwagiliaji na kuzalisha mchele kwa vile vinu vya ukoboaji vya NAFCO vingeendelea kutumika tu. Serikali au vyama vya ushirika vya hawa wakulima vingeweza hata kuvikarabati. Pia nielewavyo ni kwamba mtu akilima sehemu ya ardhi kwa muda mrefu (kama squatter), sheria inaruhusu ifanywe ni mali yake halali. Mbona kwa watu hawa sheria hii haitumiki?

Kama sera na maamuzi ya CCM ni kukumbatia wakubwa wawili wanaoweza kuchukua hekta elfu sita kila mmoja, basi huo ni uamuzi wa kutia mayai yote katika kapu moja (au mawili?) Nielewavyo ni kuwa wakulima wengi kati ya hawa “wakodishaji” walikuwa wana hekta kama 50 au chini ya hapo. Maelezo kuwa wawekezaji hawa wapya “walionunua” watatuongezea ajira si sahihi kwa vile hata hawa “wakodishaji” walikuwa wanaajiri wasaidizi. Naamini wafanyakazi wa hawa wawekezaji wawili watakuwa kama manamba tu, badala ya kuwa wasaidizi.

Licha ya kwamba sina utaalamu wa kukadiria thamani ya ardhi, naona kwamba hekta hizi 13,400, yaani eka 30,016 za mashamba haya ya Mbarali na Kapunga zimeuzwa kwa wawekezaji kwa jumla ya shilingi billioni 5.811. Huu ni wastani wa Shillingi 193,597 kwa kila eka. Je hii ni bei ya ardhi katika kanda hii ya nchi yetu?

Sitaki kujiingiza katika malumbano na ubishi na Mhe. Waziri Mungai kwa vile ana majukumu mengi mno, lakini nasisitiza kuwa ni haki yangu kutoa maoni yanayohusu maendeleo ya nchi yangu hata kama maamuzi yenyewe yamefanywa na Serikali iliyochaguliwa. Maamuzi yanayogusa maisha ya wananchi yanachambuliwa na yeyote aliye ndani au nje ya Bunge na hivyo si uchochezi. Mwisho kwa Mhe. Mungai kusema eti nigawie wananchi wenye ardhi ndogo shamba langu kama naona huruma kwao, ni kushindwa kujibu hoja na mjadala ulio mbele yetu. Mjadala ni jinsi ya kuhifadhi mazingira kwa maendeleo ya Watanzania wengi iwezekanavyo.

Kwa taarifa ya wasomaji, shamba langu la kahawa lina hekta 20 (eka 52.16) tu. Lilikuwa linamilikwa na mzungu kabla sijalinunua, na hakuna hata mwananchi mmoja aliyehamishwa kunipisha! Hata hivyo namkaribisha Mhe. Mungai kulitembelea aone kilimo cha kisayansi na matumizi bora ya maji ya kumwagilia, mambo ambayo nashauri wakulima wa Mbarali wangesaidiwa kuendeleza. Majirani zangu wa Arumeru wanalitembelea mara kwa mara na kuona mfano.

Mwisho naomba wasomaji wa makala hii, kwa heshima na taadhima, waamue kama kweli inaashiria kuzeeka kwangu vibaya kama huyu Mheshimiwa Waziri anavyodai katika Taarifa yake kwa Vyombo vya Habari. Namkumbusha Mhe. Mungai kwamba yeye na mimi tulikuwa wote na nyadhifa za juu wakati wa Awamu ya Kwanza na naendelea kumheshimu.

Mungu ibariki Tanzania.


 
lf.curl lf.curl2 rt.curl2 rt.curl