Hivi karibuni niliandika makala yenye ‘Sera ya majimbo na siri ya Maisha bora kwa kila mtanzania’. Wengi wamenipigia jumbe mbalimbali za kunipongeza. Wengine wameniuliza maswali na baadhi wamepingana na hoja zangu. Lengo la makala yangu ya leo ni kujibu baadhi ya maswali hayo na kufafanua dhana na muktadha wa baadhi ya hoja nilizozitoa.
Nafurahi kwamba kuna waliopingana na hoja zangu si kwa sababu tu ya kubisha, ila wameingia katika viatu vya watanzania wenye hofu kuhusu majimbo ama wanaopotoshwa kuhusu majimbo. Na ni kweli kabisa. Na hasa baada ya kuzindua sera ‘nzito’ (heavy) kwenye uchaguzi na tena kuanzia kuitambulisha Kilimanjaro! Washindani wetu wakaitumia hii fursa kupotosha sera hii na kuwatia hofu wananchi. Uzuri ni kwamba hakukuwa na hoja zilizotolewa, zaidi ya kauli tu ni ‘ukabila’, italeta vita kama Nigeria, ni Ubaguzi, wengine watakosa rasilimali nk. Sasa tuna miaka mitano ya kubishana kwa hoja. Na niliwahi kusema huko nyuma ukweli ukitamalaki aliyesema uwongo hutamani kujifunika kwa kiganja kama Adili na nduguze. Na hii ndiyo itawakumbuka viongozi wa juu wa CCM miaka kadhaa toka sasa. Changamoto kwetu sasa ni kuuhamisha mjadala huu kwa wananchi ili wafahamu undani wa mambo haya. Na ninavyoona sasa kuna masuala ambayo tumeanza kuelewana.
Wapo waliotoa hoja kwamba tusifanye kitu kwa kuiga!. Ukweli ni kwamba hii haikuwa sera ya kuiga. Ilizuka kama wazo (idea) tu, kwamba kwa kuwa falsafa yetu ni nguvu ya umma, kwa nini tusipeleke mamlaka kwa umma. Tukajiuliza ni kwa njia gani, likaja wazo la kuwa na mfumo mpya wa utawala-ikiwemo suala la muundo mpya wa utawala (majimbo). Na kwa kweli ilikuwa ni eneo jipya kiasi kwamba kulikuwa na mitazamo tofauti kuhusu mfumo uweje. Katika harakati hizo ndio tulipoanza kuangalia pia je nchi nyingine zinafanyaje? (hii inakaribia na kuiga). Lakini hatukuingia kiundani sana kuchota mifano ya nchi nyingine kwa kuwa hata muda huo hatukuwa nao. Kwa hiyo tukafikiria kwa kadiri ya mazingira yetu. Tukaingia kwenye uchaguzi. CCM wakaanza kupotosha kwa kutumia mifano ya nchi mbalimbali. Hapo sasa ikabidi kuingia kiundani hiyo mifano wanayoitoa kwa nia ya kuwajibu, hapo ndipo mjadala sasa kwa pande zote ukaanza kutawaliwa na mifano ya nje(hapa ndipo hisia za kwamba tunaiga zikaanza kujengeka). Lakini nilisema na narudia-sisi tulikuja na dhana ya uliberali/umajimbo wa kiutendaji (functional federalism).
Wapo waliojenga hoja kinzani kwamba nchi nyingi wanachukua ufiderali kwa sababu ya kutafuta UMOJA. Nakubaliana nao. Lakini UMOJA ni sababu moja tu. Hata sisi ni moja ya sababu kama msingi mmoja wapo (rejea makala yangu ya awali). Lakini kila nchi ni zaidi ya hapo, pitia misingi ya ufiderali ya nchi mbalimbali utakubaliana na mimi.
Mchambuzi mmoja amechukua muda mrefu kupinga hoja zangu kwa kuzungumzia mfano wa Afrika Kusini na ubaguzi wa rangi (Apartheid). Kwa kufanya hivyo, nami hapa chini nitatoa uchambuzi wangu kuhusu Afrika Kusini. Hoja kubwa iliyotolewa ni kwamba Afrika Kusini (SA) wamechukua muundo wa majimbo ili kukabiliana na ubaguzi wa rangi (apartheid), na kwamba palikuwa na majimbo manne katika nchi hiyo ambayo yamegawanyika. Nakubali kuwa palikuwa na majimbo manne (kwa hiyo kama ingekuwa ni kwa lengo la kuunganisha majimbo kuleta umoja na kuondoa ubaguzi pekee kwa nini Afrika Kusini imeamua kuwa na majimbo tisa badala ya hayo manne?) Haya majimbo mengine matano yametoka wapi?Yameundwa kwa vigezo gani? Nitajadili suala hili kiasi hapo chini.
Wengine wamenijia huu na kusema kwamba hawakubaliani nami kama mipaka yetu imewekwa kiubaguzi. Kwanza niseme kwamba sijatamka bayana kwamba mipaka yetu imewekwa kiubaguzi. Nilichosema ni kwamba imetokea mara kadhaa watawala wetu kuweka mipaka ya kiwilaya bila kutoa sababu za kina na kuonekana kuwa ni kwa misingi ya ukabila ama makabila. Niliwauliza maswali mawili ambayo kwa kuwa sikupewa majibu ya kina nimeona leo niyaulize rasmi kupitia makala yangu: “Unaweza ukaniambia ni kwanini Rais ameigawa wilaya ya Tarime kuwa wilaya mbili za Tarime na Rorya? Au unaweza kuniambia kwa nini wilaya ya Hai ambayo ni ndogo iligawanywa kuwa wilaya mbili za Hai na Siha (wilaya ambayo kwa idadi ya watu ni ndogo kuliko hata kata moja yenye watu wengi zaidi katika jimbo la Ubungo)?”
Mchambuzi mmoja ametoa hoja kwamba hatuna sababu ya kuweka mistari ya uwanja wa mpira wa kikapu (basketball) ilihali tunacheza mpira wa miguu (football). Na mchambuzi amehitimisha hoja yake kwa kuuliza kwa lugha ya kiingereza sera ya majimbo ‘for what’ ambayo naweza kutafsiri “kwa ajili gani ama kwa nini?’ Hii ni njia nzuri ya kujenga hoja kwa kutumia mifano, nami nitautumia mfano huu kufafanua hoja za awali. Hapa kuna mambo mawili-Mosi, ni kwamba hii mistari tunayoita mistari hivi sasa ilichorwa na watu kama sisi (ila wao tunawaita watawala). Mistari ya nchi ilichorwa na wakoloni. Baadhi ya mistari ya mikoa na wilaya tukairithi toka kwao. Na mistari mingine watatawala wakaanza kuichora. Na mingine wanaendelea kuichora. Mwaka juzi wakachora mstari kukatokea mkoa unaitwa Manyara. Na sasa nasikia wanataka kuichora zaidi. Wasiwasi wetu ni kwamba wanaichora vibaya, bila shabaha (hawajibu swali FOR WHAT). Sisi tunataka ichorwe na wananchi kupitia mchakato wa kuunda katiba mpya. Iwe mistari ya wananchi kwa ujumla wao na kwa matakwa yao. Tunaweka wazi misingi ya ufiderali. Halafu kwa pamoja tuamue uweje na mipaka yake iweje. Tunapotaja mipaka ya maeneo hivi sasa mathalani ya Jimbo la Ziwa ama Jimbo la Kaskazini nk tunataja kama mawazo yetu tu na ili kurahisha uelewa. Mipaka itakuwa ipi hili ni suala la wananchi kuamua. Tofauti na sasa ambapo Rais anaweza akalala akaamka akatangaza kugawa mkoa....na akateua anayemtaka kuwa mkuu wa mkoa ama akafanya hivyo kwa wilaya..Hakuna udhibiti, hakuna urari, hakuna ushiriki(No checks, No balance, No participation)....FOR WHAT, anaweza tu kuwajibu kwamba URAIS HAUNA UBIA, AMA NIMEFANYA HIVYO KWA MASLAHI YA UMMA, AMA NIMEFANYA HIVYO KWA MAMLAKA MLIYONIPA!
Mmoja ameandika kulalamika kwamba sera ya majimbo itaibagua “Singida”. Nadhani Singida imetumika kama ishara (symbolic) ikimaanisha maeneo ambayo hayana raslimali. Mambo kadhaa yanajitokeza. Mosi, hakuna haja ya kufikiria sana kuhusu Singida-hakutakuwa na Jimbo linaitwa Singida, Singida ni mkoa wa hivi sasa ambao utavunjwa na kuunganishwa na maeneo mengine kuwa na JIMBO LA KATI (central province). Itajumuisha maeneo gani itategemea idadi ya majimbo nchi nzima kwa mujibu wa uamuzi wa wananchi. Lakini kama tukiwa na majimbo 8 au 9 basi Jimbo la Kati linaweza kuwa na Maeneo ya DODOMA, SINGIDA, MTERA, KILOSA nk. Sasa wakazi wa maeneo haya watuambie je, kanda hii itakuwa haina rasilimali? Huku kuna Zabibu, Mabwawa ya Maji, Mito, Mbuga za wanyama, Ardhi ya Kilimo nk. Lakini nirudie ambacho niliwahi kukisema, na nakirudia tena-duniani kote RASLIMALI ni zaidi ya MALIASILI. Kuna majimbo (states) hazina MALIASILI lakini zinatumia RASLIMALI watu na upekee wake kufanya kwenda mbele. Kadiri Singida inavyoendelea kuwa tegemezi kwa Dar es salaam (Soma-serikali kuu) msitegemee maajabu ya Mussa. Hivi mpaka sasa DODOMA imetumiaje fursa ya kuwa Mji Mkuu wa Bunge kuleta maendeleo? (Hapa namaanisha, Dodoma sio mji mkuu wa Tanzania- huu ni mjadala mwingine tofauti-Ni wapi kwenye katiba pameandikwa kwamba mji mkuu ni Dodoma ama ni lini sheria ya bunge ilipitishwa kubadili makao makuu ya nchi kuwa Dodoma zaidi ya sheria njiti iliyoibuka baadae ya Mamlaka ya Maendeleo ya Mji Mkuu (CDA)?
Nimelalamikiwa kwa kutumia mifano ya nchi zilizofanikiwa. Nadhani ni kitu kizuri kutumia mifano mizuri na kujifunza kutoka katika mifano mibaya. Wachambuzi watupe nchi ambazo zimeshindwa kutokana na kutumia Mfumo wa Ufiderali. Nami nitatoa mifano ya nchi nyingi zaidi zilizofanikiwa kutokana na ufiderali na nchi zilizoshindwa kutokana na serikali kuu kuhodhi kila kitu (unitary).
Yupo aliyesema kwamba Nigeria haiendelei kutokana na majimbo. Wanaojua historia na mwelekeo wa nchi watakubaliana nami kwamba yanayotokea Nigeria si kwa sababu ya majimbo, tena ukweli ni kwamba kuna majimbo ambayo yamepitisha sheria za imaendeleo (progressive laws) zinazowapa wananchi wake manufaa ya raslimali. Kuna majimbo ambayo hayana msalie mtume na rushwa. Harakati (Struggle) za Niger Delta si kati ya wananchi kwa wananchi, ni kati ya wananchi na watawala waliofunga ndoa na makampuni ya kinyonyaji. Ni struggle ambayo hata Tanzania inakuja, tuwe na mfumo wa ufiderali, tusiwe nayo hatuwezi kuwazuia wananchi kudai raslimali zao. Njia pekee ni kutambua hili kama tatizo la kiungozi na kulishughulikia. Na kwa kweli muundo wa sera ya majimbo (in herent) unatambua suala la wananchi kumiliki ama kunufaika na raslimali kama nilivyodokeza katika makala yangu iliyopita.
Sasa nirudi kwenye mfano wa Afrika Kusini. Nchi hii imepitia mchakato wa kuwashirikisha wananchi katika kuunda katiba yao tofauti na katiba ya Tanzania hivyo uamuzi wa majimbo ni wa wananchi. Nao ndio walioamua kuwa na majimbo tisa badala ya manne. Na ni kwa kuangalia sababu za ukubwa wa kimaeneo, raslimali, historia, mamlaka nk. Na hili si suala geni, Canada kwa mfano ilibuni mfumo wake wa majimbo mwaka 1867 (kwa sababu za umoja zaidi), lakini majimbo ya Canada yamekuwa yakibadilika, ama kuongezeka au wajibu wake kubadilika kutokana na mageuzi ya kijamii, ukubwa, dhima ya serikali na maamuzi ya kimahakama. Hii inathibitisha kwamba majimbo ya kiutendaji (functional federalism) sio ndoto. Ni kitu kinawezekana kwa lengo la kukidhi matakwa fulani (the FOR WHAT). Matakwa ambayo mimi nimeyaanisha kwenye misingi tisa niliyoitoa katika makala yangu iliyopita.
Chama ambacho kilikuwa kinapambana na ubaguzi wa rangi Afrika Kusini ni African National Congress (ANC). Kwa hiyo kama nia ya kuunda majimbo ingekuwa ni kupambana na ubaguzi wa rangi, ANC ingekuwa ya kwanza kutaka mfumo wa MAJIMBO/UFIDERALI. Lakini ANC ilikuwa inapinga majimbo(kama walivyo rafiki zao CCM wa Tanzania). Na walikuwa wanasema wanataka Mamlaka ya Serikali Kuu (Unitary government) ili serikali kuu ya chama tawala ANC iweze kutoa huduma kwa wananchi kila mahali mathalani hospitali, shule na kuondoa tofauti za kiuchumi (hii ni hoja ambayo kwa kutamkwa ni tamu!).
Na ANC (kama ambavyo CCM inafanya sasa) ilikuwa ikisambaza propaganda kwamba neno FEDERALISM (MAJIMBO) ni la kibaguzi na kimbari na kwamba linafanana na HOMELANDS, neno lililokuwa linayagawa maeneo kwa mujibu wa ubaguzi wa rangi (Ndio maana haishangazi kwamba kwenye katiba ya Afrika Kusini hakuna neno FEDERALISM ingawa nchi hii imeundwa, inatambua na kufuata mfumo wa UFIDERALI). Lakini nakubaliana na uchambuzi kwamba katika yale majimbo manne ya asili yapo ambayo yalikuwa yakitaka kujitenga mathalani KwaZULU Natal. Lakini mwisho wa siku wananchi waliuopenda zaidi mfumo wa ufiderali.
Mwalimu alitaka Serikali ya Mamlaka (unitary government)-hoja zake zilikuwa hizo hizo za serikali kuu kupeleka huduma kila mahali. Ametimiza wajibu wake katika wakati wake. Kuna mahali amefanikiwa, kuna mahali ameshindwa. Sasa, zimepita nyakati za dola kuhodhi uchumi (state centralized economy). Sasa ni wakati wa watu (namaanisha wazawa na si wageni) kumiliki uchumi (people centred economy). Na huu ndio msingi wa falsafa ya nguvu ya umma na itikadi ya mrengo wa kati!. Na hili nimelichambua katika misingi ya ufiderali ambao CHADEMA inapendekeza Tanzania tuufute. Ndio maana naendelea kusisitiza kuwa pamoja na kuwa kipaumbele ni UONGOZI kuna uhusiano mkubwa baina ya MFUMO/MUUNDO WA UONGOZI na UONGOZI wenyewe. Na hili ndilo nashauri serikali inayoongozwa na CCM ilizingatia. Kama haitalizingatia basi wananchi wanapaswa kujulishwa mapema kwamba wakichagua CHADEMA wanachagua falsafa ya NGUVU YA UMMA kutumika katika utawala na UFIDERALI kuwa muundo- labda kama wananchi (ambao sio wote wanaunga mkono sera za CHADEMA) au bunge (ambalo halitakuwa la CHADEMA peke yake)-WAKATAE wakati wa mjadala wa KATIBA MPYA! Wakati huo tutaamua kama tufuate Ufiderali uliogawanyika (divided federalism) kama ilivyo Canada ama tufutate Ufiderali uliounganika (integrated federalism) kama ilivyo Ujerumani. Naamini maoni yangu haya yataibua mjadala zaidi tuendelee kujadili, wananchi wengi zaidi wafahamu ukweli ili tukubaliane ama tukubaliane kutokukubaliana.