lf.bevel
MWANZO CHAMA SERA KATIBA TUUNGE MKONO UCHAGUZI TUWASILIANE
banner

16 Mei 2007

Waraka kwa Watanzania (1)

na
Freeman Aikaeli Mbowe

LEO napenda kuelekeza waraka na tafakuri yangu kwa Watanzania wote.

Rais wetu ana majukumu mengi na ni busara nimpe nafasi, kwa nia njema, atafakari kama akipenda, yale yote niliyoainisha kwenye tafakuri na nyaraka zangu kwake.

Waraka wangu leo haumlengi yeyote kipekee, bali unakusudia kutoa ufafanuzi wa jambo moja la msingi. Hakika, kama yupo mwenye uelewa zaidi na mwenye kuamini maelezo yangu, leo ni ya kupotosha, ingekuwa busara ajitokeze na aseme, “Mbowe unadanganya.”

Katika waraka wangu namba sita kwa Rais wetu, Jakaya Kikwete, niliouandika kupitia gazeti hili la siku ya Jumatano Mei 9, 2007, niliainisha sehemu tu ya ukubwa wa gharama zinazotokana na safari za rais nchi za nje.

Ukubwa wa gharama zile zimeonekana kushtua baadhi ya watu. Mimi nasema, gharama nilizoainisha ni sehemu tu na wala si gharama kamili zinazotumika kwenye safari hizi. Aidha, muungwana mmoja alinisihi nisome ufafanuzi uliotolewa na Mheshimiwa Waziri Mkuu wakati akifunga mkutano wa saba wa Bunge kule Dodoma, Mei 20, mwaka huu, kwani ingeweza kuondoa hofu yangu. Namshukuru sana.

Kwa bahati mbaya hata hivyo, hoja ya muungwana huyu haikuwa majibu rasmi toka serikalini. Mara nyingi nimeomba ufafanuzi wa hofu zinazojengeka, ili pengine tusiwajengee viongozi wetu taswira hasi mbele ya jamii. Wao mara nyingi wamechagua “kula jiwe”. Tutaendelea kuwakumbusha pale inapobidi, kwani ndio wajibu wetu sisi watawaliwa.

Hoja ya muungwana huyu, inaweza vilevile kuwakilisha fikra zilizofichama za viongozi wetu, wasaidizi au wapambe wao. Hata kama hawatasema kwa kauli, ukimya au muendelezo wa vitendo hivyo bila kuonyesha dalili ya kuvijutia, ni kiashiria tosha kuwa fikra za muungwana zaweza kushabihiana na zao.

Tafsiri rahisi ni kuwa, ni vigumu kwa yeyote asiye mbia kwa njia moja au nyingine kudiriki kuushabikia na kuhalalisha ufujaji wa kiwango hiki kwa nchi masikini mithili ya Tanzania.

Pengine kwa faida ya tafakuri ya leo, na uelewa wa wasomaji, ninukuu maneno yaliyokuwa sehemu ya hotuba ya Waziri Mkuu, Edward Lowassa wakati akifunga mkutano wa saba wa Bunge kule Dodoma Aprili 20, 2007 kwa mujibu wa kumbukumbu za Bunge, (hansard). Nanukuu:

“Mheshimiwa Spika,
Katika mkutano huu yametolewa maelezo ndani ya Bunge lako tukufu kuhoji safari za Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nje ya nchi. Napenda kutoa ufafanuzi ufuatao wenye lengo la kueleza umuhimu wa ziara za Mheshimiwa Rais nje ya nchi kwa maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika,
Awali ya yote, ningependa kufahamisha waheshimiwa wabunge na wananchi wote kwa ujumla kuwa, ziara anazofanya Mheshimiwa Rais nje ya nchi ni za kikazi na zenye malengo maalum. Matokeo ya ziara hizo yameanza kuonekana yakiwa na faida kubwa kwa nchi yetu. Naomba nitoe mifano michache:

Mwezi Septemba 2006, Mheshimiwa Rais alitembelea nchi ya Marekani. Akiwa nchini Marekani, Mheshimiwa Rais alifanya mazungumzo na Rais wa Marekani na kutokana na mazungumzo hayo, rais wetu ameahidiwa kupata msaada kutoka Millenium Challenge Corporation.

Tanzania itanufaika kwa kupatiwa msaada wa jumla ya fedha ya dola za Kimarekani milioni 800 kwa ajili ya kuendeleza miradi ya maendeleo katika sekta za barabara, maji na nishati.

Msaada huu umeweka rekodi miongoni mwa nchi za Afrika ambapo awali nchi iliyokuwa ikipata fedha nyingi kutoka Marekani ni Ghana ambayo imepata dola za Kimarekani milioni 500.”

Nakubaliana na Waziri Mkuu kuwa, kuna umuhimu wa rais kusafiri nje kwa majukumu yake. Waziri Mkuu angetusaidia zaidi Watanzania kama angetoa maelezo ya ziada kujibu yafuatayo:

Mosi, ni nini hasa gharama halisi za safari za rais na za viongozi wa juu serikalini? Pili, kuna ulazima gani rais kuandamana na msafara mkubwa ilhali nchi yetu ikiomba misaada kila kukicha?

Tatu, kuna ulazima gani wa kusafirisha msafara katika madaraja ya juu ya ndege ilhali safari zenyewe zikiwa za kwenda kuomba misaada?

Nne, kuna sababu gani za msingi kulaza misafara hii katika mahoteli ghali mno wakati serikali yetu ikiwa haina uwezo hata wa kugharamia bajeti yake yenyewe?

Maadam Waziri Mkuu alitoa mfano wa safari hii ya rais kuwa ilituwezesha kupata msaada wa dola za Marekani milioni 800 baada ya mazungumzo na Rais Bush, pengine nieleze taarifa toka vyanzo vingine zinazoonekana kukinzana na ile ya Waziri Mkuu kuhusu hiki kinachoelezewa kuwa matunda ya safari ya rais nchini Marekani mwezi Septemba 2006.

Kati ya mwaka 2002 na 2004, Serikali ya Marekani chini ya utawala wa Rais George W. Bush, uliunda Shirika la Millenium Challenge Cooperation (MCC) kwa lengo la kusimamia mfuko maalum uitwao Millenium Challenge Account (MCA). Vyote hivi vinaratibiwa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani.

Mfuko huu una kusudi la kusaidia nchi masikini zaidi duniani kujiimarisha kimaendeleo. Tofauti na misaada mingine inayotolewa na wafadhili, vigezo vitatu vikuu vimewekwa na Marekani ili nchi husika ziweze kuingizwa kwenye mpango huu. Vigezo hivyo ni: Utawala wa haki, mipango ya maendeleo yenye kulenga rasilimali watu na sera na mipango ya kiuchumi yenye kuzingatia uhuru wa kiuchumi wenye kulenga kufungua milango ya biashara na uwekezaji.

Mwezi Novemba 2005, chini ya utawala wa Rais Benjamin Mkapa, Tanzania sambamba na nchi nyingine 22, zilifuzu kufaidika na mfuko huu kwa vigezo vilivyotajwa. Aidha ilikidhi sifa ya msingi ambayo ni umasikini wa kipato kwa watu wake.

Kwa mantiki hii, si kweli kuwa safari ya Rais Kikwete ya mwezi Septemba 2006 ndiyo iliyozaa mpango huu. Katika ziara ya Septemba, rais alikutana na Rais Bush hotelini kwa muda usiozidi dakika 15 na dhahiri haukuwa muda wa kutosha kusalimiana, kupeana taarifa, kuombana misaada na kisha kukubaliana.

Aidha, ni vyema tukajenga utamaduni kama wa wenzetu, ambapo mambo yanayohusu majukumu na mipango ya serikali huwa wazi na kamwe si siri kama inavyolazimishwa katika nchi yetu.

Pamoja na Tanzania kuingizwa kwenye mpango huu, mwaka 2005 wakati Kikwete akiwa katikati ya kinyang’anyiro cha uchaguzi mkuu, Tanzania ilionekana kugubikwa na tatizo kubwa la rushwa jambo lililochukuliwa kuwa ni kikwazo cha msingi katika mipango ya kuleta maendelo endelevu nchini.

Kutokana na udhaifu huu, Tanzania iliruhusiwa kuandaa kwanza mpango maalum wa awali wa kupambana na rushwa chini ya kinachoitwa “threshold program”. Iliahidiwa kupewa dola za Marekani milioni 11.15 chini ya usimamizi wa USAID ili kujenga mfumo wa kukabiliana na rushwa kabla ya kuweza kupata fungu kuu, ambalo tumeahidiwa kama tukikamilisha vigezo na masharti mengine.

Mkataba wa msaada huu wa aibu, ulisainiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Gray Mgonja kwa niaba ya Tanzania na Pamela White, Mkurugenzi wa USAID Tanzania, Mei 3, 2006, kufuatia kupitishwa rasmi kwa mpango huu wa awali na Bodi ya MCC Januari 27, 2006.

Rais Jakaya Kikwete naye, akiwa ziarani nchini Marekani, Mei 17, 2006 alihudhuria hafla fupi ya kuzindua mradi huu unaoonyesha kuwapo kwa kasoro wa kukabiliana na rushwa nchini kwetu, katika hafla iliyofanyika jijini Washington, Marekani.

Sherehe hiyo vilevile ilihudhuriwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa mfuko huo, balozi John Danilovich, Kaimu Afisa Mtendaji wa USAID, Fredrick Schiek na Katibu wa Hazina ya Marekani, Joln Snow. Balozi wa Marekani nchini Tanzania Michael Retzer na balozi wa Tanzania (wakati huo) nchini Marekani, Andrew Daraja walihudhuria sherehe hiyo.

Nauita mkataba huu wa “threshold program” wa aibu, kwani unathibitisha rushwa yetu, tena ya kujitakia, inavyojulikana kimataifa kuwa ni kigezo kinachokwamisha maendeleo ya nchi yetu. Viongozi wetu wanapodhihakiwa kwa kupewa msaada ili wakasafishe serikali ni aibu kwa taifa na wala si jambo la ujemedari na kujisifia! Ni dhahiri kuwa, serikali yetu haijashindwa kupata dola milioni 11.15 kupambana na rushwa bali tatizo limekuwa kukosekana dhamira.

Katika mkataba huu wa aibu, serikali yetu imeahidi katika kipindi cha miaka miwili hadi ifikapo Juni 30, mwakani, kufanya mambo yafuatayo:

Mosi, kuweka mfumo unaohakikiki manunuzi katika halmashauri zisizopungua 60 nchi nzima.

Pili; kuongeza uwezo wa Takuru kusimamia kesi angalau kati ya 20 mpaka 28 mahakamani katika kila halmashauri.

Tatu; kuongeza uwezo wa vyombo vya habari kuweza kuibua kashfa za rushwa na hivyo kuongeza kesi za asili hiyo kutoka 50 kwa sasa hadi 300.

Nne; kuanzisha na kujenga kitengo cha uchunguzi cha “finance intelligence unit”, kiweze angalau kuchunguza kashfa nzito za fedha zisizo za kawaida; kuweka mpango wa ukaguzi wa angalao idara na wizara zisizopungua 40 za serikali na taarifa hizo kutangazwa kwenye vyombo vya habari.

Serikali yetu bado haijataka kuzungumzia kwa uwazi na kwa kina aibu hii zaidi ya kusema kuwa ni msaada unaolenga kujenga utawala bora!

Sambamba na “threshold program”, Tanzania imeruhusiwa kutengeneza kinachoitwa “country compact proposal”, ambao ni mchanganuo yakinifu unaoeleza ni miradi gani inayokusudiwa kufanywa katika sekta tatu zilizokubaliwa kimsingi kufadhiliwa, ambazo ni miundombinu (dola milioni 387), maji (dola milioni 243) na nishati (dola milioni 131). Utawala wa mradi huu nao umetengewa dola milioni 39; zote jumla zikiwa dola milioni 799.2 za Marekani.

Tangu kusainiwa kwa mkataba wa “threshold program”, yapo masharti mengine kadhaa yameendelea kutolewa na Marekani ili kuwezesha Tanzania kupata msaada huu. Mengine ni ya heri na mengine ni kitanzi kwa wananchi, hasa wale masikini. Zipo hata sheria kadhaa zinatungwa kama sehemu ya masharti haya na wananchi hawaambiwi ukweli wa chimbuko lake.

Baadhi ya sheria zilizoshinikizwa na msaada huu ni ‘Anti Money Laundering Act’ sambamba na uundwaji wa ‘Financial Intelligence Unit’ na sheria mpya za barabara (Roads bill 2007) na sheria ya kuzuia rushwa ya mwaka 2007.

Kadhalika, baadhi ya masharti yanayoambatana na msaada huu, ni pamoja na kuitaka Tanroads kuongeza fungu kwa ajili ya matengenezo ya barabara kuwa asilimia 40 ya bajeti yake.

Masharti mengine ni pamoja na kuwa na mkakati wa taifa wa nishati (National energy stratergy), Tanesco kujiendesha na kujitegemea kifedha, sheria ya umeme kurekebishwa ili kuondoa ukiritimba wa Tanesco, kuongeza bei ya umeme ili Tanesco iweze kujiendesha na kujitegemea na ZECO (Zanzibar Electricity Company) walipe viwango vya kibiashara kwa umeme wanaopata Tanesco.

Mengi ya heri yamefanywa na serikali katika mpango huu. Ni dhahiri mipango kadhaa inayopendekezwa na serikali katika mpango huu inahitaji kupongezwa na kuungwa mkono, kwani pamoja na mambo mengine imeelekezwa zaidi katika maeneo ambayo kwa hakika yanahitaji kufikiriwa kwa kila njia inayowezekana.

Hii ni pamoja na kusudio la ujenzi wa barabara za Tunduru – Songea; Peramiho – Mbamba Bay; Tunduma – Sumbawanga; Manyoni – Itigi – Tabora; Kigoma – Kasulu – Kibondo – Nyakanazi; Tanga – Horohoro; upanuzi wa uwanja wa ndege wa Kigoma na Mafia na barabara za Zanzibar vijijini.

Upande wa miradi ya maji, msaada huu unategemewa pamoja na mambo mengine usaidie kuboresha au kuweka mifumo ya maji katika mikoa ya Dar es Salaam, Bukoba, Zanzibar Mjini, miji ya Pemba na Morogoro. Makusudio mengine ni pamoja na Bunda, Bariadi, Same, Misungwi, Tarime, Geita na Zanzibar Vijijini.

Yapo mapendekezo kadhaa ya miradi ya umeme maeneo mbalimbali nchini. Hata hivyo, kwa mujibu wa vyanzo vya uhakika vya habari, miradi ya nishati ina hofu kubwa ya kufadhiliwa kwa sababu kadhaa zikiwamo; hofu ya uendeshaji wa Tanesco, kukosekana uwazi katika jinsi serikali inavyotoa ruzuku kwenye sekta ya nishati na kukosekana kwa mkakati kitaifa wa nishati.

Pamoja na serikali kuonekana kupata kigugumizi, hasa katika kukabiliana na rushwa, jambo linalozua hofu kwa wafadhili wetu kama kweli serikali ina nia na dhamira thabiti ya kupambana na rushwa, nawajibika kuipongeza serikali kwa jinsi wataalam wake wamejibidisha kwa nguvu kujaribu kutekeleza vigezo kadhaa kuwezesha nchi yetu kupata msaada huu utakaosaidia watu wengi, ukipatikana kwa ukamilifu wake.

Tunaitaka serikali isifanye mzaha hata kidogo kwani rushwa ndiyo hadi sasa inachelewesha utoaji wa kiwango kilichoahidiwa. Serikali nayo isiendelee kutia taifa hili aibu ya kuonekana limejaa wala rushwa kwa wao kufanyia masihara ahadi zake!


lf.curl lf.curl2 rt.curl2 rt.curl